Vyama vya Ushirika vyaombwa kununua hisa KCBL |Shamteeblog.

Na Safina Sarwatt, Moshi

Vyama vya Ushirika wa Mazaoa (AMCOS), vimeombwa kuona umuhimu wa kuwekeza kwa njia ya kununua hisa za benki yao kwa zaidi ya asilimia 51.

Mwenyekiti wa Bodi ya KCBL, Dk. Gervas Machimu, ameyasema hayo Februari 19, 2021 mjini Moshi mkoani Kilimanjaro wakati akisoma taarifa yake kwa Katibu wa Kilimo Gerald Kusaya, alipoitembelea benki hiyo.

Dk. Machimu amesema Benki ya Ushirika ya KCBL, inatarajia kuuza hisa zake asilimia 86 ikiwa ni hisa milioni 172.505, zenye thamani ya Sh bilioni 86.252.

Aidha Dk. Machimu amesema benki hiyo imepitisha mchakato wa kuanza kutafuta wawekezaji mbadala wakiwemo wa vyama vya ushirika, watu, taasisi na jumuiya za kimataifa, zilizopo nchini na wananchi wenye mapenzi mema kuwekeza kwa njia ya kununua hisa za benki hiyo.

Awali, akizungumza Meneja wa Benki ya Ushirika KCBL, Godfrey Ngura, amesema asilimia 86 ya hisa zilizopo kwenye benki hiyo hazijauzwa na kunaviomba vyama vya ushirika kuona umuhimu wa kuwekeza ndani ya benki yao kwa lengo la kununua hisa hizo.

Nae, Mrajisi wa Vyama Vya Ushirika nchini na Mtendaji Mkuu wa Tume ya Maendeleo ya Ushirika nchini, Dk. Benson Ndiege, aliwataka watumishi wa benki hiyo kuwa na nidhamu wakati wa utendaji wa majukumu yao.

“Ninawaomba sana Watumishi muendelee kuwa na nidhamu ya utendaji kazi wenu, wakati mwingine tunaweza kuanza kuhujumiana humu sisi kwa sisi kama serikali hatuwezi kushindwa kumjua anayetuhujumu, na kama tutambaini sheria kali atachukuliwa dhidi yake,”alisema Dk. Ndiege.

Aidha, Dk. Ndiege aliwapongeza wafanyakazi wa KCBL kwa kuwa na moyo wa uvumilivu wa miaka mitatu bila kulipwa mshahara wowote lakini waliendelea kuwepo katika benki hiyo.

Kwa upande wake Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo, Gerald Kusaya, amewataka KCBL kujipanua zaidi hata mteja aliyeko Mtwara, Simiyu, Ukerewe na Mbozi, aweze kupata huduma ya KCBL bila hata kuliona jengo la KCBL lilipo.



from Author

0/Post a Comment/Comments

Previous Post Next Post